Parish Details
HISTORIA YA PAROKIA YA
YESU KRISTO KUHANI MKUU WA MILELE - BWIRU
UTANGULIZI:
Parokia teule ya Bwiru
ilianza kama kigango mnamo mwaka 1995, kikiwa chini ya Parokia ya Familia
Takatifu Pasiansi. Katika chimbuko hili, ni Padre Bromius ambaye katika utume
wake alipata kuasisi kigango hiki kwa wakati ule. Aidha, ni katika kazi zake za
kitume ambapo miaka hiyo vigango vya Nyang’wilolelwa na Pasiansi kwa nyakati
tofauti viliasisiwa. Katika kuimarika na kukua kwa imani kigango cha Bwiru,
kilirasimishwa na kufunguliwa/kuwekewa jiwe la msingi na Hayati Askofu Mkuu
Antony Mayala wa Jimbo kuu la Mwanza mnamo tarehe 12/ 01/2002. Aidha,
tarehe 28/05/2018, Kigango kilipandishwa hadhi na kuwa Parokia
teule na Askofu Mkuu Yuda Thadei Ruwa’ichi wa Jimbo kuu Mwanza (wakati huo).
MAPADRE WALIOWAHI KUHUDUMU
Katika historia, kanisa
kwanza linawashukuru mapadre wote waliowahi kutoa huduma za kiroho. Wamechangia
kulikuza na kuimarisha imani kwa waamini. Padre Bromius, Janusz, Segayamu,
Julius, Patrick, John Baptist, Antony Gill, Patrick Machayi, Joseph Chege, na
kwa sasa Parokia Teule ikihudumiwa na Pd. Josephat Nzioka (Paroko), Pd.
Jeremiah Bitiong na Pd. Chewe Mweshi (maparoko wasaidizi); na wengine wote
ambao hawajatajwa kwa namna moja au nyingine na kwa nyakati tofauti katika
kutoa huduma. Mwenyezi Mungu awabariki sana kwa utume wao.
VIONGOZI HALMASHAURI
WALEI WAANZILISHI:
Ndugu Originos Lopa, Respicius Bishubo, Felichismi Mwijage, mzee Kirumo; kwa nyakati tofauti wameongoza kigango hiki. Mpaka kigango kupata hadhi ya kuwa Parokia Teule, viongozi hawa wamefanya kazi ya utume na kufanikiwa kuzaa kigango cha Mt. Antony wa Padua – Kitangiri, na sasa Parokia teule ikiwa na Halmashauri ya walei na Joseph Kachwele (M/kiti), Jires C. Damian (makamu M/kiti), Esther Bundala - Katibu, Fidelis Rwiza-Katibu msaidizi na Winfrida Mutta-M/hazina. Kanisa linawashukuru sana viongozi wote waliotangulia na kuonyesha njia katika kuyatakatifuza malimwengu. Mwenyezi Mungu awabariki sana.
JUMUIYA:
Wakati kigango
kinaasisiwa kilikuwa na jumla ya Jumuiya mbili (2) tu; Mt. Petro na Mt. Antony
wa Padua. Mungu ni mwema, mpaka leo Parokia teule inazinduliwa ziko jumla ya
Jumuiya kumi na tano (15) na vigango viwili (2).
MAENDELEO YA KANISA:
Parokia yetu teule
imepiga hatua kadhaa za maendeleo. Ni msingi pekee kuwa huduma mbalimbali za
Jumuiya, ubatizo, kipaimara, ndoa, misa za katikati ya juma na kila juma na
huduma zote za kanisa; ni maendeleo ambayo yamepelekea leo kuwa na hadhi rasmi
ya kuzinduliwa kuwa parokia. Aidha, kutoka kusali darasani, kukalia madawati,
tofali na sasa kuwa kanisa rasmi ni hatua. Hata hivyo, ununuzi wa kiwanja
(square metre 17,400) cha kujenga kanisa la Parokia; ni hatua nyingine ya
maendeleo na leo kupewa hadhi hii ya kuwa Parokia kamili..
UPATIKANAJI WA KIWANJA
CHA KANISA:
Tunawashukuru baadhi ya
ndugu zetu mzee Kizwalo, Mama Mati na mzee Sabuni ambao kwa moyo wa
dhati walikubali kutuachia kiwanja hiki, kwa fidia kidogo ambayo walilipwa.
Tunawashukuru sana pia; mama Amina Masenza (mkuu wa wilaya wakati huo), m/kiti
serikali ya mtaa - mama Kingu, Afisa ardhi wilaya Ilemela (wakati huo), mama
Diana Maijo, mama Sungura, Moshi Mstafa, mama Gwanchele wakishirikiana na Respicius
Bishubo, Andrew Bundala, Remi Ndesanjo na Victor Kiruma; kwa namna
walivyofanikisha katika upatikanaji wa eneo / kiwanja hiki.
SHUKRANI:
Tunakushukuru sana Baba
Askofu Mkuu, Renatus Nkwande, kwa kuridhia leo hii na kuipandisha hadhi ya kuwa
Parokia kamili. Mungu akubariki sana katika utume wako. Akupe afya njema ya
akili na mwili katika majukumu yako ya kila siku.
MWISHO:
Tunawashukuru sana, tena sana kwa dhati kabisa walezi wetu Parokia
ya Familia Takatifu – Pasiansi. Walikubali kuwa wazazi, na kweli wametufunda
katika malezi mema, mpaka leo kuwa Parokia ni kwa sababu ya mapenzi na utashi
mwema walio nao katika kutulea na kuhakikisha misingi ya kiimani tunaishi na
kuimarika kwa waamini wa Bwiru. Wametusaidia katika mengi, tunasema ahsanteni
sana Pasiansi.